WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

Sunday 26 October 2014

WAZIRI CHIKAWE ATANGAZA KUTETEA JIMBO LAKE



Na Felix Mwagara, Nachingwea
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Mathias Chikawe ametangaza rasmi kuwa atagombea tena katika nafasi ya ubunge kupitia CCM katika uchaguzi Mkuu ujao na kulitetea jimbo lake.
Alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na wananchi pamoja na viongozi wa CCM wa Wilaya na Kata ya Mtua katika sherehe ya kuwapokea viongozi na wanachama wapya wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) waliojiunga na CCM wilayani humo.
Chikawe alisema wananchi wake bado wanamuhitaji kwa hiyo hawezi kuacha kugombea nafasi hiyo kwani wazee na wananchi mbalimbali katika Kata zote alizokuwa akipita kufanya mazungumzo nao wanamuomba agombee tena nafasi hiyo.
“Ninyi wenyewe mashahidi mmewasikia viongozi pamoja na wananchi wanavyosema kuwa bado wananihitaji kwa hiyo siwezi kuacha wakiwa bado wana mapenzi na mimi kiongozi wao,” alisema Chikawe na kufafanua kuwa;
“Muda ukifika nitachukua fomu ya kugombea ili niendelea kuliletea maendeleo makubwa jimbo letu ambalo mpaka sasa lina mabadiliko makubwa tangu nilipoanza kuliongoza mwaka 2005, ninyi wote ni mashahidi na mmeona mabadiliko hayo ndiyo maana mmefikia hatua ya kuniomba niendelee kuliongoza jimbo hili.”
Chikawe alisema wakati akiingia ubunge jimboni humo kulikuwa na hakuna lami na barabara nyingi za kwenda vijijini zilikuwa hazipitiki na pia maji yalikuwa shida lakini sasa barabara za lami mjini Nachingwea zimejengwa, maji yanapatikana tena yasio na chumvi, barabara vijijini zinapitika kwa kuwa zimechongwa vizuri kwa kuwawezesha wakulima kupitisha mazao yao.
“Sitaweza kuwadharau ndugu wananchi na pamoja na viongozi wenzangu wa CCM Nachingwea, nimekubali kugombea tena nafasi hii ya ubunge na kuwaahidi wilaya yetu kuwa na mabadiliko makubwa zaidi,” alisema Chikawe huku akishangiliwa na mamia ya wananchi waliofurika katika sherehe hiyo ya CCM.
Wakati huohuo, Waziri Chikawe alimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Regina Chonjo, mabati 2,000 kwa ajili ya ujenzi wa maabara katika shule 20 za Sekondari za Kata jimboni humo.
Aidha, katika sherehe hiyo, Chikawe aliwapokea wanachama 23 wa CHADEMA kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambapo wanachama hao walirudisha kadi zao na kupewa kadi za CCM pamoja na kuvalishwa sare za chama hizo.
Kati ya wananchama hao, pia kulikuwa na viongozi wa Chadema Wilaya ambao ni  Mjumbe wa Kamati Tendaji ya Wilaya ya Nachingwea, ambaye pia ni Kaimu Mwenyekiti wa Umoja wa akina Mama wa Chadema wilayani humo, Manufreda Malenga pamoja na Katibu wa Siasa Kata ya Mtua, Habibu Oswadi.
Mwisho/-

No comments:

Post a Comment