JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA
YA MAMBO YA NDANI YA NCHI
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
Waziri wa Mambo ya Ndani ya
Nchi, Mhe. Charles Kitwanga amesema zoezi linaloendelea sasa la kukamata raia
wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi hapa nchini bila vibali halitawagusa wageni
wenye vibali halali.
Mheshimiwa Kitwanga ameyasema
haya mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na jumuiya ya raia toka nchini China
wakati wa sherehe zilizoandaliwa na raia hao katika Hoteli ya Golden Tulip jijini
Dar es Salaam.
Katika sherehe hizo ambazo
ziliandaliwa mahsusi kuukaribisha mwaka Mpya wa Kichina, Mheshimiwa Kitwanga
alisema uhusiano wa Tanzania na China ulianzishwa na marehemu Baba wa Taifa
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Kiongozi wa China, marehemu Mao Zedong zaidi
ya miaka hamsini iliyopita.
Amesema uhusiano huo
umeendelea kuimarishwa hadi katika nyanja za kiuchumi ambapo hadi sasa kuna
zaidi ya Kampuni 500 za Kichina ambazo zinafanya shughuli za kibiashara hapa
nchini ambazo zimetoa zaidi ya nafasi 100,000 za kazi kwa Watanzania.
Mheshimiwa Kitwanga alitumia
fursa ya sherehe hizo kuwahakikishia wawekezaji wote waliopo hapa nchini kuwa
Serikali ya Tanzania italinda biashara zao kufuatana na sheria za nchi.
Kuhusu zoezi linaloendelea
hapa nchini la kukamata wageni ambao wanaishi na kufanya kazi bila vibali
halali alisema kumekuwa na taarifa za uzushi zinazoenezwa hapa nchini na nje ya
nchi kuwa Serikali ya Tanzania inawafukuza wageni kwa vile haihitaji raia wa
kigeni hapa nchini.
Amesema taarifa hizo ni za uongo
zinazolenga kuichafua Tanzania katika jumuiya ya kimataifa na kusema raia wa
kigeni wanaokamatwa ni wale tu wasio na vibali halali vya kuishi na kufanya
kazi hapa nchini.
Amesema zoezi hilo ni la
kawaida na linafanywa kufuatana na Sheria za Uhamiaji lakini halitawahusu
wageni wenye vibali halali vya kufanya kazi na kuishi nchini.
Kati ya mwaka 2014 na
Januari 2016 Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imetoa vibali vya ukaazi kwa
jumla ya wageni 40,765 toka mataifa mbalimbali na idadi hiyo inaendelea kuongezeka
siku hadi siku.
Wageni waliofukuzwa kwa
sababu mbalimbali mwaka 2015 ni 1,642.
Aidha, kati ya 08 Desemba,
2015 na 14 Januari, 2016 raia wa kigeni waliokamatwa kwa kuishi na kufanya kazi
nchini bila vibali halali ni kama ifuatavyo:
1.Burundi 284
2.Kenya 26
3.Uganda 13
4.Somalia 7
5.Ethiopia 157
6.DRC 34
7.China 285
8.India 41
9.Zambia 40
10.Nigeria 08
11.Lebanon 01
12.Ivory Coast 10
13.Madagascar 05
14.Malawi 27
15.Korea 09
16.Zimbabwe 01
17.Ghana 01
18.Rwanda 03
19.Afrika Kusini 01
20. Wenye uraia wa utata 11.
Kati ya hawa, wengine
wamemepelekwa katika kambi za wakimbizi, hasa raia waliotokea Burundi, wengine
wamepewa amri ya kuondoka nchini na wengine kesi zao ziko katika hatua
mbalimbali mahakamani.
MWISHO
(Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano ya
Serikali, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi – 24 Januari, 2016)
No comments:
Post a Comment