WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

Thursday 19 June 2014

SIKU YA WAKIMBIZI DUNIANI KUADHIMISHWA TAREHE 20 JUNI, 2014




JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

SIKU YA WAKIMBIZI DUNIANI KUADHIMISHWA
TAREHE 20 JUNI, 2014
Tarehe 20 Juni ya kila mwaka ni siku ya Wakimbizi duniani na kwa Tanzania  siku hiyo itaadhimishwa kitaifa hapa Dar es Salaam katika Hotel ya Sea Cliff, ambapo mgeni rasmi katika halfa hiyo atakuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Mathias Chikawe.
Kufuatana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni “Familia moja kusambaratika na vita ni wengi mno” au kwa Kiingereza “1 family torn apart by war is too many”.
Taarifa hiyo inaongeza kuwa kiasi cha watu 43 milioni duniani kote wamelazimika kuyahama makazi yao kwa sababu ya vita, machafuko au majanga ya asili, na kati yao kiasi cha milioni 10 wanahudumiwa na Shirika hilo.
Kwa upande wa Tanzania, kiasi cha wakimbizi wapya wanaoomba hifadhi imepungua ilikinganishwa na miaka ya nyuma ambapo kuna wakati idadi yao ilikaribia kufikia milioni moja.  Kupungua huku ni ishara ya kuimarika kwa hali ya usalama ndani ya nchi walizotoka wakimbizi hao, hususan nchi za eneo la Maziwa Makuu.  Hata hivyo, bado hali si shwari sana mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), hali inayosababisha baadhi ya raia wa nchi hiyo kuikimbia na kwenda kuomba hifadhi ya ukimbizi katika nchi nyingine ikiwemo Tanzania.
Mfano wa mafanikio yaliyopatikana hapa nchini kuhusiana na suala la Wakimbizi ni kufungwa kwa kambi za wakimbizi zaidi ya kumi na mbili ambapo kambi ya mwisho kufungwa ya Mtabila iliyokuwa wilayani Kasulu mkoani Kigoma iliyokuwa na raia zaidi ya 35,000 toka Burundi ilifungwa mwishoni mwa Desemba, 2012.  Sasa hivi Tanzania imebakiwa na kambi moja tu ya Nyarugusu, wilayani Kasulu mkoani Kigoma ambayo ina wakimbizi takribani 65,084, wengi wao wakiwa ni kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi na Jumuiya ya Kimataifa linaamini suluhisho la kudumu kwa tatizo la wakimbizi ni kwa wakimbizi kupata nafasi ya kurejea kwao kwa hiari, mara baada ya mazingira yaliyowafanya kuzikimbia nchi zao kutoweka.  Jambo hili litafanyika na kufanikiwa pale Serikali za nchi na Jumuiya ya Kimataifa zitakapochukua hatua za makusudi kuhakikisha kuwa sababu zinazowafanya raia wa nchi mbalimbali kuzikimbia nchi zao zinatafutiwa ufumbuzi.  Hii ni pamoja na kuwa na Serikali zinazozingatia sheria, utawala bora na haki za binadamu.

Imendaliwa na:  Isaac J. Nantanga – Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
19 Juni, 2014

No comments:

Post a Comment