WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI

Sunday 20 July 2014

Waziri Chikawe amwaga misaada ya mabati 100 na jezi za mipira Nachingwea

Felix Mwagara, Nachingwea
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Nachingwea, Mathias Chikawe ametoa msaada wa mabati 100 kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Nditi pamoja na jezi za mpira wa miguu kwa timu sita zilizopo katika kata hiyo, jimboni kwake Nachingwea mkoani Lindi jana.
Waziri Chikawe pia ametoa mifuko 15 ya Saruji kwa ajili ya ujenzi wa Msikiti uliopo katika Kata hiyo pamoja na kuwataka wananchi washirikiane kufanya kazi ili kuiletea maendeleo kata yao ambayo ni moja ya kata ni muhimu katika Jimbo lake la Nachingwea.
Akizungumza baada ya kutoa msaada huo pamoja na kusikiliza kero mbalimbali za viongozi wa Kata ya Nditi katika mkutano na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Kata hiyo, Wajumbe wa Mabaraza wa Jumuiya zote za CCM Kata, Viongozi wa Dini na Wajumbe wa Baraza la Wazee wa Kata alisema chama chake CCM kipo bega kwa nega na wananchi ikiwa na lengo la kuwaletea maendeleo zaidi.
“Nafurahi leo (jana) kuzungumza na viongozi wa Kata hii, nimekuja hapa kusikiliza kero zenu ambazo mnazijua ndani ya kata hii, hata hivyo nimezisikiliza kupitia hotuba yenu pamoja na maswali mbalimbali mlioniuliza, na tayari baadhi ya maswali yenu nimeyajibu na mlichokuwa mnahitaji nimewasaidia,” alisema Chikawe.
Chikawe aliongeza kuwa, licha ya kuendelea kutoa misaada ya kijamii mbalimbali katika jimbo lake lakini pia amepanga kukuza michezo katika jimbo hilo ambapo ameanza kwa kutoa msaada wa jezi kwa timu sita za mpira wa miguu katika Kata ya Nditi na baadaye atahamia katika kata zingine za jimboni kwake.
“Michezo ni muhimu kwa afya na pia muhimu kwashughulisha vijana hawa, maana kuna msemo usemao ‘Usipowashughulisha vijana hawa watakuja kukushughulisha, sasa ngoja tuwashughulishe kabla ya kutushughulisha,” alisema Chikawe.
Akizungumza baada ya kupokea msaada wa jezi za mpira wa miguu, Afisa Mtendaji wa Kata ya Nditi, Patrick Mwasambungu alimshukuru Waziri Chikawe kwa msaada huo na jezi hizo atazigawa kwa timu hizo katika kata yake.
Aidha, Chikawe aliwataka viongozi hao kutoa elimu zaidi kwa wananchi wao endapo rasimu ya pili ya Katiba ikipitishwa na Bunge la Maalum la Katiba washiriki kikamilifu katika kupiga kura ya maoni kwani Katiba ndio msingi wa maisha ya kila Mtanzania na muelekeo wa nchi yetu. 
Waziri Chikawe yupo jimboni kwake Nachingwea kwa ziara maalum ya kuzungumza na viongozi wa CCM katika kata zake pamoja na kusikiliza kero mbalimbali zinazowasibu katika kata zao.
Mwisho/-

No comments:

Post a Comment